VITA YA MBATIA NA MREMA YAZIDI KUSHIKA KASI

Mwenyekiti wa chama cha NCCR Mageuzi James Mbatia (kushoto) akiteta jambo na Mwenyekiti mwenza wa TLP Augustin Mrema.

Vita ya ubunge baina ya wenyeviti wawili wa vyama vya upinzani, James Mbatia na Augustine Mrema imezidi kupamba moto baada ya kushambuliana bungeni kuhusu kusigana kwenye harakati za ubunge wa Jimbo la Vunjo..

Kwenye vikao vya Bunge na nje, Mrema, mwenyekiti wa TLP, amekuwa akimlalamikia Mbatia (NCCR-Mageuzi) kuwa anamuingilia kwenye jimbo lake, lakini juzi alikwenda mbali zaidi alipoomba kuwasilisha taarifa ya hali yake kiafya na kutumia nafasi hiyo kumshambulia mpinzani wake, ambaye pia jana aliomba nafasi kama hiyo kujibu mapigo.
Msuguano wa wawili hao, ambao waliwahi kuwa pamoja kwenye Chama cha NCCR, ulitokana na uamuzi wa Mbatia kutangaza nia ya kugombea ubunge wa Vunjo, jimbo ambalo kwa vipindi viwili limekuwa chini ya Mrema.
Mrema ambaye pia amewahi kuwa mbunge wa Jimbo la Temeke, alisoma taarifa hiyo ya hali yake ya afya akisema kuwa yeye si mgonjwa kama inavyodaiwa na atagombea tena ubunge kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka huu.
Katika taarifa yake aliyoimbatanisha na ripoti za madaktari kuhusu vipimo alivyofanya na ambayo alitumia dakika 15 kuisoma, Mrema alimtuhumu Mbatia kwamba amevamia jimbo hilo na kuwaambia watu wasiwachague wagombea wa TLP, akiwamo na yeye (Mrema) kwa sababu ni marehemu mtarajiwa, ana saratani na Virusi vya Ukimwi.
Akieleza jinsi Rais Jakaya Kikwete na Spika Anne Makinda walivyofanikisha safari zake za kwenda nchini India, kuchunguzwa afya yake, kutibiwa saratani ya mapafu pamoja na kupima Ukimwi, Mrema alisema: “Awali nilikuwa na saratani ya mapafu, lakini baada ya kupata matibabu kwa mwaka mmoja, nimepima tena na ripoti za madaktari zinaonyesha kuwa nimepona.
“Nilipima na ukimwi na vipimo vimeonyesha sina maambukizi yoyote. Kweli Mungu mkubwa. Hafi mtu hapa. Mimi ni mzima wa afya na nitagombea ubunge maana ndiyo unanitoa roho.”
Hata hivyo, Mbatia, ambaye ni mbunge wa kuteuliwa na Rais, jana jioni alikanusha madai hayo bungeni akisema hayana ukweli wowote.





Credit; Mwananchi
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment