UCHAGUZI 2015; UKAWA WAANZA SAFARI



Wakati CCM ikisubiri Februari kufanya tathmini kuona kama baadhi ya wagombea wake wa urais wametekeleza masharti ya adhabu zao, washindani wao wa Ukawa,
Jumanne ijayo watakutana kujadili mambo mbalimbali, ukiwamo mchakato wa kuwapata wagombea wake wa urais, ubunge na udiwani, imefahamika.
Tangu mwaka huu uanze zimekuwapo pilikapilika nyingi za kisiasa ndani ya vyama vya siasa na Jumanne iliyopita CCM ilifanya kikao cha Kamati Kuu mjini Zanzibar na kutoa maazimio yanayogusia mchakato huo lakini ikasita kutaja ratiba rasmi ya mchakato wa kuwapata wagombea wa CCM.
Wakati hali ikiwa hivyo, habari zilizopatikana na kuthibitishwa na baadhi ya viongozi wa Ukawa, umoja huo utakutana jijini Dar es Salaam Januari 20, ukiwa na ajenda mbalimbali kuhusu ushirikiano wao, likiwamo suala la kupata wagombea huku vikao vya ndani ya vyama vikitarajiwa mwishoni mwa mwezi huu.
Mwenyekiti Mwenza wa Ukawa, James Mbatia alithibitisha jana kuwapo kwa kikao hicho Jumanne akisema kutakuwa na ajenda nyingine lakini: “Suala la kupata wagombea nalo huenda likajadiliwa. Kuhusu suala la mgombea urais wa Ukawa, linaweza kuwa sehemu ya mazungumzo lakini halipo kwenye ajenda.”
Ajenda nyingine alizotaja ni mwongozo wa Ukawa, kura ya maoni ya Katiba, changamoto za uandikishaji wa daftari la wapiga kura, hali ya uchumi na tathmini ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliomalizika Desemba mwaka jana. Mbatia, ambaye pia ni Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi alisema watajadili ajenda hizo ili kuhakikisha wanatafuta majibu ya changamoto zilizopo kwa sasa.
Kiongozi huyo pia alithibitisha taarifa kuwa kila chama ndani ya Ukawa kupitia vikao vyake kitateua majina ya wagombea ambao watashindanishwa ndani ya umoja huo, akisema kabla ya Machi, jina la mgombea urais ndani ya chama chake litakuwa limeshapendekezwa.
Awali, Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Mosena Nyambabe alisema vikao vya chama hicho vinavyotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi huu vitakuwa na ajenda ya uchaguzi vitakavyojadili mwelekeo wa uchaguzi huo kama kalenda yake inavyosema.




Credit; Mwananchi
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment