IKULU YATOA TAMKO KUHUSU PROFESA MUHONGO

Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu Salva Rweyemamu akiongea na waandishi wa habari.

Ikulu imewataka Watanzania kuacha kulichukulia suala la kujiuzulu kwa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo kama jambo la ‘kufa na kupona’, huku ikieleza kuwa waziri huyo mpaka sasa bado ni kiongozi wa Serikali.

Akizungumza na waandishi wa habari Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Salva Rweyemamu alisema hatua zilizochukuliwa kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi aliyesimamishwa kazi kupisha uchunguzi haziwezi kuwa sawa na za Profesa Muhongo kwa sababu Maswi ni mtumishi wa Serikali na profesa huyo ni mwanasiasa.
Rweyemamu alitoa ufafanuzi huo baada ya kubanwa na wanahabari waliotaka kujua sababu za Profesa Muhongo licha ya kuwekwa kiporo na Rais Jakaya Kikwete kutokana na kuhusishwa na kashfa ya uchotwaji wa Sh306 bilioni katika Akaunti ya Tegeta Escrow, bado anafanya shughuli mbalimbali za Serikali, ikiwa ni pamoja na juzi kwenda kuhudhuria mkutano nchini Uswisi.
“Utaratibu wa kumwajibisha yeye (Muhongo) ni tofauti na wa Maswi. Kama mtakumbuka Bunge lilitoa maazimio yake ambayo bado yanaendelea kutekelezwa. Msilichukulie suala hili kama la kufa na kupona,” alisema Rweyemamu.
Akizungumzia kauli hiyo, Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika alisema, “Kauli hiyo ya Ikulu inadhihirisha udhaifu wa Rais. Rais alisema anamweka kiporo kwa siku mbili, Ikulu inapaswa kueleza ni kwa nini Rais ameamua kumweka kiporo zaidi ya siku hizo mbili wakati alidai kuwa kuna uchunguzi mdogo tu.
“Kwa namna wanavyomlinda Muhongo na watuhumiwa wengine, naendelea kutoa wito kwa wabunge wenzangu tusaini hoja ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu kwa kuwa kwa kufanya hivyo, baraza la mawaziri litavunjika na hivyo kiporo cha Muhongo na mizigo mingine ndani ya baraza la mawaziri itaondoka.”
Katika kikao cha 16 na 17 cha Bunge, Bunge kupitia azimio lake la pili liliazimia kwamba Waziri wa Nishati na Madini, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini na Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Tanesco wawajibishwe kwa kuishauri mamlaka yao ya uteuzi kutengua uteuzi wao.
Kati ya wote waliolengwa katika azimio hilo ni Profesa Muhongo pekee ambaye mpaka sasa bado hajawajibishwa na mamlaka yake ya uteuzi.
Jaji Frederick Werema ambaye alikuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali alijiuzulu, Maswi alisimamishwa kazi, Profesa Anna Tibaijuka aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi alifutwa kazi huku Bodi ya Tanesco ikiundwa nyingine.




Credit; Mwananchi
Share on Google Plus

About Unknown

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments :

Post a Comment